Upepo mkali ukiambatana na mvua umeezua nyumba 44 katika 
Kijiji cha Kiemba Kata ya Ifulifu, Wilaya ya Musoma mkoani Mara. 
Kati ya
 nyumba hizo, tano ziliathirika vibaya kiasi cha kusababisha wamiliki 
wake kulala nje. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo 
alikagua baadhi ya nyumba zilizoathirika ili kuona athari za uharibifu 
huo. 
Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dk Vicent Naano na viongozi wa 
halmashauri, walitembelea eneo hilo baada ya kupata taarifa za athari za
 kuezuliwa paa na kuagiza tathmini ifanyike ili Serikali iweze kutoa 
msaada kwa wananchi hao. 
Profesa Muhongo aliwaambia waathirika hao 
kuwa Serikali ya Rais John Magufuli ipo pamoja nao na ametumwa kuwapa 
pole kutoka kwa viongozi wa juu wa Serikali. 
“Ndugu wananchi, nimetumwa na Rais wetu Dk John Magufuli niwape pole sana kwa kukutwa na 
kadhia hii ya kuezuliwa na upepo kwa paa za nyumba zenu. Makamu wa Rais 
na Waziri Mkuu wanawapa pole pia na wanawatakia heri wale wote 
walioathirika,” alisema. 
Profesa Muhongo aliwaelekeza viongozi wa 
kijiji hicho wahakikishe wanafanya tathmini ya kweli kwa kupita kila 
nyumba iliyoathirika na yoyote atakayegundulika amedanganya ili Serikali
 imlipe, zoezi zima litaahirishwa na kurudiwa upya, pia wahusika 
watachukuliwa hatua za kinidhamu. 
Aliwaahidi wananchi hao kuanza kupewa 
misaada baada ya kikao cha halmashauri kupitia taarifa ya tathmini 
kesho, na kuwaelekeza viongozi kufanya kazi hiyo kwa haraka. 
Profesa 
Muhongo alikuwa mkoani Mara kwa ziara ya kikazi ya kukagua umeme na 
kushiriki maadhimisho ya kumbukumbu ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius 
Nyerere iliyofanyika nyumbani kwake Butiama juzi. 


0 Comments
on