Walimu
 wa Shule ya Sekondari Hasanga, iliyopo wilayani Mbozi mkoani Songwe na 
wafanyabiashara wawili, wanahojiwa na vyombo vya usalama mkoani Mbeya 
kwa tuhuma za kuhusika na utengenezaji wa mitihani feki ya kidato cha 
nne.
Watuhumiwa
 hao, James Kapinga (36) ambaye anadaiwa kufanya kazi Shule ya Sekondari
 ya Hasanga pia anajitolea kufundisha Shule ya Sekondari ya Wazazi ya 
Sangu, Baraka Mwazambe (28), mfanyabiashara na mkazi wa Tunduma na 
mtaalamu wa masuala ya Tehama (IT), Alex Mochi.
Watu
 hao kwa pamoja inadaiwa walikamatwa juzi usiku baada ya mwanafunzi 
mmoja ambaye jina lake na la shule vimehifadhiwa kukutwa na mtihani wa 
somo la Kiingereza na alipobanwa, inadaiwa aliwataja wahusika hao.
“Mwanafunzi
 huyu ni wa shule nyingine tena si ya Mbeya, alikutwa na mtihani feki wa
 somo la Kiingereza, alipohojiwa alieleza mtihani huo ulitoka Mbeya na 
Serikali ilipofuatilia iliwabaini wahusika ambao walikuwa wanasambaza 
mitihani feki,” kilisema chanzo kimoja cha habari hii.
Akizungumzia
 sakata hilo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Mariamu Mtunguja, alikiri 
ofisi yake kupokea taarifa juu ya uvujaji wa mitihani na walipofuatilia 
walibaini mitihani hiyo ni feki.
“Mbeya
 hakuna mitihani iliyovuja kama inavyoelezwa katika mitandao, ukweli ni 
kwamba suala hilo lilifuatiliwa ilibainika mitihani inayosambazwa si ile
 iliyochapishwa na Baraza la Mitihani la Taifa, ni feki na baadhi ya 
wahusika wanahojiwa na vyombo vya dola,” alisema.
Naye Kaimu Ofisa Elimu Mkoa wa Mbeya, Benedict Sandy, alisema hakuna mitihani iliyovuja.
“Mitandao
 imekuwa ikitoa taarifa za upotoshaji eti mitihani imevuja, mitihani 
iliyosambaa na kukutwa na baadhi ya wanafunzi tena si wa Mkoa wa Mbeya 
ni feki na wahusika wanaodaiwa kuisambaza wamekamatwa.
“Nawaomba
 wanafunzi wazingatie yale waliyofundishwa, mitihani hiyo inakuja kwa 
lengo baya la kuwapotezea muda wao na mwisho wa siku kuishia kufeli, 
watu wanaofanya kazi hiyo wapo kimasilahi,” alisema.
 
 


 
 
 
 
 
0 Comments
on